Judges 20

Waisraeli Wapigana Na Wabenyamini

1 aNdipo Waisraeli wote kuanzia Dani hadi Beer-Sheba na wa kutoka nchi ya Gileadi wakatoka kama mtu mmoja wakakusanyika mbele za Bwana huko Mispa. 2 bViongozi wote wa kabila za Israeli wakakaa kwenye nafasi zao katika kusanyiko la watu wa Mungu, askari 400,000 waendao kwa miguu wenye panga. 3(Wabenyamini wakasikia kuwa Waisraeli wamepanda kwenda Mispa.) Ndipo Waisraeli wakasema, “Tuelezeni jinsi jambo hili ovu lilivyotendeka.”

4 cHivyo yule Mlawi, mume wa yule mwanamke aliyeuawa, akasema, “Mimi na suria wangu tulifika Gibea ya Benyamini ili tulale huko. 5Wakati wa usiku watu wa Gibea wakanijia na kuizingira nyumba, wakitaka kuniua. Wakambaka suria wangu mpaka akafa. 6 dNdipo nikamchukua suria wangu, nikamkatakata vipande vipande na kuvipeleka katika nchi yote ya urithi wa Israeli, kwa kuwa wametenda uasherati mkubwa na jambo la aibu katika Israeli. 7 eSasa, ninyi Waisraeli wote, semeni na mtoe uamuzi wenu.”

8Watu wote wakainuka wakasema, kama mtu mmoja, “Hakuna hata mmoja wetu atakayekwenda nyumbani. Wala hakuna hata mmoja wetu atakayerudi nyumbani kwake. 9 fSasa hili ndilo tutakaloitendea Gibea: Tutaikabili jinsi kura itakavyotuongoza. 10Tutatoa watu kumi katika kila 100 kutoka kwenye kabila zote za Israeli, watu 100 katika watu 1,000 na watu 1,000 katika 10,000, ili waende wakalete mahitaji kwa ajili ya jeshi. Basi wakati jeshi litakapofika Gibea ya Benyamini, watawatendea yale wanayostahili, kwa ajili ya uovu huu wa aibu waliotenda katika Israeli.” 11Hivyo wanaume wote wa Israeli wakakutanika pamoja na kujiunga kama mtu mmoja dhidi ya huo mji.

12 gMakabila ya Israeli yakatuma watu kwenda katika kabila la Benyamini lote na kuwaambia, “Ni uovu gani huu wa kutisha uliotendeka katikati yenu? 13 hBasi watoeni hao watu waovu kabisa walioko Gibea, ili tupate kuwaua na kuondoa uovu katika Israeli.”

Lakini Wabenyamini hawakuwasikia ndugu zao, Waisraeli.
14Wakatoka katika miji yao, wakakutanika Gibea ili kupigana na Waisraeli. 15Siku ile Wabenyamini wakakusanya watu 26,000 kutoka miji yao, waliojifunga panga, mbali na hao 700 waliochaguliwa miongoni mwa hao waliokaa Gibea. 16 iMiongoni mwa hao askari wote kulikuwa na watu 700 bora waliochaguliwa watumiao mkono wa kushoto, kila mmoja wao aliweza kutupa jiwe kwa kombeo na kulenga unywele mmoja bila kukosa.

17Nao watu wa Israeli, mbali na hao wa Benyamini, wakakusanya watu waume 400,000, wenye kutumia panga, wote hao walikuwa mashujaa.

18 jWaisraeli wakapanda Betheli na kumuuliza Mungu, “Ni nani miongoni mwetu atakayetangulia mbele yetu ili kupigana na Wabenyamini?”

Bwana akawajibu, “Yuda ndiye atakayetangulia.”

19Asubuhi yake Waisraeli wakaamka na kupiga kambi karibu na Gibea. 20Waisraeli wakatoka kupigana na Wabenyamini, nao Waisraeli wakajiweka kwenye nafasi zao katika vita dhidi yao huko Gibea. 21Wabenyamini wakatoka Gibea na kuwaua watu 22,000 wa Israeli siku ile. 22Lakini Waisraeli wakatiana moyo kila mmoja na mwenzake, nao wakajiweka kwenye nafasi zao katika vile vita mara ya pili mahali pale walipokuwa wamejiweka mara ya kwanza. 23 kWaisraeli wakapanda mbele za Bwana na kulia mbele zake mpaka jioni, nao wakamuuliza Bwana wakisema, “Je, tupande tena kupigana vita na Wabenyamini, ndugu zetu?”

Bwana akajibu, “Pandeni mkapigane nao.”

24Ndipo Waisraeli wakawakaribia Wabenyamini siku ya pili. 25Wakati huu, Wabenyamini walipotoka Gibea ili kupigana nao, wakawaua watu Waisraeli 18,000, wote wakiwa wamejifunga panga.

26 lNdipo Waisraeli, watu wote, wakapanda Betheli, huko wakakaa mbele za Bwana wakilia. Wakafunga siku ile mpaka jioni na kutoa sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya amani kwa Bwana. 27 mNao Waisraeli wakauliza kwa Bwana. (Katika siku hizo Sanduku la Agano la Mungu lilikuwa huko 28 nna Finehasi mwana wa Eleazari, mwana wa Aroni, alikuwa anahudumu mbele za hilo Sanduku.) Wakauliza, “Je, tupande kwenda vitani kupigana tena na Wabenyamini ndugu zetu, au la?”

Bwana akajibu, “Nendeni, kwa kuwa kesho nitawatia mikononi mwenu.”

29 oBasi Waisraeli wakaweka waviziao kuizunguka Gibea. 30Kisha Waisraeli wakapanda kupigana na Wabenyamini katika siku ya tatu na kujiweka kwenye nafasi zao dhidi ya Gibea kama walivyokuwa wamefanya hapo kwanza. 31 pWabenyamini wakatoka ili kukabiliana nao, Waisraeli wakawavuta Wabenyamini watoke katika mji. Wakaanza kupigana na kuua watu wapatao thelathini wa Israeli, kama walivyofanya nyakati nyingine, katika njia kuu, moja iendayo Betheli na nyingine Gibea.

32Wabenyamini wakafikiri, “Wanapigwa mbele yetu kama hapo kwanza.” Waisraeli wakasema, “Sisi na turudi nyuma ili tuwavute wauache mji waende kuelekea barabarani.”

33 qWatu wote wa Israeli wakaondoka kwenye sehemu zao na kujipanga huko Baal-Tamari, nao wale waviziaji wa Waisraeli, wakatoka hapo walipokuwa kwenye uwanda wa magharibi ya Gibea. 34 rNdipo watu 10,000 bora waliochaguliwa katika Israeli wote, wakaja kuishambulia Gibea. Vita vilikuwa vikali sana, hata Wabenyamini hawakutambua kuwa maangamizi yalikuwa karibu nao kwa kiasi hicho. 35 sBwana akawashinda Wabenyamini mbele ya Waisraeli na siku ile Waisraeli wakawaua Wabenyamini watu waume 25,100, wote wakiwa wenye kujifunga silaha za vita. 36 tHivyo Wabenyamini wakaona kuwa wamepigwa.

Basi Waisraeli walikuwa wameondoka mbele ya Wabenyamini, kwa sababu Waisraeli waliwategemea hao waviziaji waliokuwa wamewaweka dhidi ya Gibea.
37 uWale waviziaji wakafanya haraka kuingia Gibea, wakasambaa na kuwaua watu wote wa mji kwa upanga. 38 vWaisraeli walikuwa wamepatana na hao waviziaji kuwa wangefanya lipande wingu kubwa la moshi kutoka huo mji, 39 wndipo watu wa Waisraeli wangegeuka kupigana.

Watu wa Benyamini walikuwa wameanza kuwapiga na kuua watu wa Israeli (wapatao thelathini), hivyo wakafikiri, “Hakika tutawapiga, kama tulivyowashinda katika vita hapo kwanza.”
40 xLakini wakati lile wingu la moshi lilipoanza kupanda kutoka ule mji, Wabenyamini wakageuka na kuona moshi wa mji mzima unapaa juu angani. 41 yNdipo watu wa Israeli wakawageukia, nao Wabenyamini wakatiwa hofu, kwa kuwa walitambua kwamba maafa yamewajia. 42Basi wakakimbia mbele ya Waisraeli kuelekea nyikani, lakini hawakuweza kukwepa vile vita. Nao watu wa Israeli waliotoka katika ile miji wakawaua huko. 43Wakawazingira Wabenyamini pande zote, wakawafuatia na kuwapata hapo walipopumzika katika viunga vya Gibea upande wa mashariki. 44 zWakaanguka Wabenyamini 18,000 ambao wote ni mashujaa. 45 aaWalipogeuka na kukimbia kuelekea nyikani hata kufikia mwamba wa Rimoni, Waisraeli wakawaua watu 5,000 wakiwa njiani. Wakawafuata kwa kasi mpaka Gidomu huko wakawaua watu wengine 2,000.

46 abSiku ile wakawaua Wabenyamini 25,000 waliokuwa mashujaa wa vita. 47Lakini watu 600 wakakimbia kuelekea nyikani katika mwamba wa Rimoni, na kukaa huko muda wa miezi minne. 48 acWaisraeli wakarudi na kuua watu wote wa Benyamini, pamoja na wanyama na kila walichokikuta. Pia kila mji waliouona waliuchoma moto.

Copyright information for SwhNEN